WAKATI sakata la ununuzi wa mitambo ya kuzalisha umeme inayomilikiwa na kampuni ya Dowans Tanzania Limited likiendelea kupamba moto, uchunguzi wa KULIKONI umebaini kuwa Serikali ya Tanzania iwapo ingeng’ang’ania kuinunua, ingeingia hasara ya karne kwani mitambo hiyo ina deni kubwa benki linalofikia dola za Marekani milioni 75 (zaidi ya bilioni 100/-).
Uchunguzi huo wa kina umebaini kwamba kati ya Aprili 30 na Novemba 9, 2007, ikiwa ni miezi kadhaa baada ya kuhaulishiwa mkataba kutoka Richmond, Dowans Tanzania Limited ilikopa fedha katika benki mbili tofauti za Barclays na Stanbic zinazofikia bilioni 97.5/- na kuiweka dhamana mitambo hiyo ya kuzalishia umeme iliyoko Ubungo na mali zote za kampuni hiyo walizonazo sasa na zote ambazo zitapatikana baadaye.
Mitambo hiyo ambayo hadi sasa ipo katika viwanja vya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) ndiyo ambayo kampuni hiyo sasa imetangaza kuiuza na mteja mkubwa alionekana kuwa ni Serikali ya Tanzania ambayo ilielezwa kuwa na nia hiyo kabla hata ya mitambo hiyo kuanza kazi.
Nyaraka ambazo KULIKONI linazo, zinaonesha kuwa Dowans walikopa jumla ya dola za Marekani milioni 55 kutoka Barclays na dola nyingine milioni 20 za Marekani kutoka Stanbic tawi la Tanzania, fedha ambazo zinapaswa kulipwa kwa riba na gharama nyinginezo.
Dowans walipokopa dola za Marekani milioni 20 kutoka Stanbic tawi la Tanzania, dhamana iliyotajwa ni mitambo ya kuzalisha umeme, akaunti yao, mikataba, bima, na amana zote za kampuni hiyo tata.
Katika mawasiliano na kampuni hiyo benki ya Stanbic yenye makao yake makutano ya Barabara ya Ali Hassan Mwinyi na Kinondoni, Dar es Salaam, iliwakilishwa na Helen Makanza na Jeff Daly wakati Dowans haionyeshi ni nani aliyewakilisha kampuni hiyo zaidi ya Wakili Samson Russumo, ambaye alikuwa Kamishna wa Kiapo.
Baadaye Juni, 2007, Dowans ilichukua mkopo mwingine wa dola za Marekani milioni 20 kutoka benki ya Barclays ya Mauritius, makubaliano yaliyoelezwa kufuata sheria za Uingereza.
Miezi minne baadaye, Dowans imebainika walichukua tena kiasi cha dola za Marekani milioni tano kutoka Barclays tawi la Tanzania, dhamana ikiwa ni mali zile zile zilizotumika kuchukua mkopo kutoka Stanbic na Barclays ya Mauritius.
Kampuni hiyo ambayo hadi sasa wamiliki wake upande wa Tanzania hawajulikani dhahiri, inaonekana katika nyaraka nyingine kuweka rehani mali zake na kuchukua dola za Marekani milioni 30, Novemba 9, 2007.
Tayari Tanesco kupitia Mkurugenzi wake Mtendaji, Dk. Idris Rashidi, imekwishajitoa kununua mitambo hiyo ya Dowans ‘kwa shingo upande’ huku ikiwatisha Watanzania kwamba watapata matatizo makubwa ya umeme kwa “kutofanya uamuzi sahihi,” huku wito wa kutaka wahusika wote walioingiza nchi katika matatizo wajiuzulu na kuchukuliwa hatua ukiendelea.
Kabla ya Tanesco kujitoa kununua mitambo hiyo, wadau mbalimbali akiwamo Spika wa Bunge, Samuel Sitta, waliitahadharisha serikali kuhusu mpango wake wa kununua mitambo ya Dowans.
Sitta aliishauri serikali kufuata ushauri wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ambayo ilipendekeza kwa serikali kuachana na mchakato wa kununua mitambo hiyo.
Tanesco walitaka kununua mitambo hiyo kutoka Dowans kwa dola za Marekani milioni 69 sawa na bilioni 90/-, kiwango ambacho kimeelezwa kwamba ni kikubwa mno na huenda kililenga kulipia deni la benki ambalo kampuni hiyo inadaiwa hadi sasa.
Tayari Dowans wamefungua mashtaka kwenye Baraza la Kimataifa la Usuluhishi Paris, Ufaransa huku Tanesco wakiwa wamefungua kesi Tanzania wakitaka mali za Dowans zizuiwe hadi hapo shauri la Ufaransa litakapokwisha.
Awali, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja naye alikaririwa akisema kwamba serikali inaunga mkono ununuzi wa mitambo hiyo ya Dowans kutokana na hali halisi ya nishati nchini na kwamba uamuzi huo ndio sahihi kwa wakati huu na hauhusiani na ufisadi wowote, kauli iliyopingwa na wadau wengi.
Miongoni mwao ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, William Shellukindo na makamu wake, Dk. Harrison Mwakyembe, ambao wote walisisitiza kwamba ukosefu wa umeme utatokana na uzembe wa uongozi wa Tanesco na si kwa kutonunuliwa mitambo ya Dowans na kwamba upo uwezekano wa kupata mitambo mipya kwa bei mwafaka.
Nyaraka zinaonyesha kwamba Kampuni ya Dowans (T) Ltd, inamilikiwa kwa asilimia 61 na kampuni ya Dowans ambayo inatajwa kuwa na makao yake nchini Costa Rica, na asilimia 39 na kampuni ya Portek, yenye makao yake makuu Singapore.
Dowans inatajwa kuhusishwa na raia wa Oman mzaliwa wa Zanzibar, Suleiman Mohamed Yahya Al Adawi, ambaye hata hivyo uhusiano yake na wanasiasa wa Tanzania unatia shaka.
Utata wa Richmond uliwaponza aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa na mawaziri wawili waliowahi kuongoza Wizara ya Nishati na Madini, Nazir Karamagi na Dk. Ibrahim Msabaha, ambao walilazimika kujiuzulu ndani ya Bunge kwa kuhusishwa kwao na kashfa ya mradi huo wa umeme wa dharura.
Hata hivyo pamoja na kuushindwa mradi huo na kuhaulisha kazi zake kwa Dowans Richmond imekuwa ikijinasibu katika tovuti yake kwa kuanzisha mradi huo na kufanya maandalizi ya sehemu kubwa ya kukamilishwa kwa mradi huo.
Maswali: Kwanini walikuwa wanashinikiza tununue mitambo hii ya Dowans? Je inajalisha kama mitambo imewekwa rehani kwenye deni/madeni ya kibenki? Je wale waliokuwa wanataka serikali (walipo kodi wa Tanzania) wanunue majenereta haya walikuwa wanajua juu ya deni hilo?
|