KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Yusuph Makamba, amewaonya viongozi wa ngazi za mikoa na wilaya nchini kuziachia Jumuiya za Umoja wa Vijana (UVCCM) kuchagua viongozi wanaowataka, badala ya kuwashinikiza kuchagua kwa matakwa ya watu binafsi.
Makamba alitoa kauli hiyo jana alipotembelea jengo la UVCCM tawi la Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) lililopo Kata ya Mbuyuni, Manispaa ya Morogoro ambalo limegharimu zaidi ya sh milioni 10.
Alisema vijana wanajua viongozi wao na hivyo hakuna sababu kuwachagulia na badala yake waachiwe vijana wenyewe kuwa na maamuzi ya viongozi wanaowataka.
“Wagombea wote wa nafasi ya mkoa ya vijana wanajulikana, hakuna sababu ya kuwatumia ujumbe vijana, ili wachague mtu mnayemtaka nyie,” alisema.
Tatizo la kuchaguliana viongozi lina madhara yake, kwani hawezi kufanya kazi ipasavyo na kutimiza malengo na matakwa ya vijana kama wanavyotarajia.
“Uchaguzi wa wilaya umemalizika kwa sasa kinachotakiwa ni kujikita katika matawi yenu, kuhakikisha shughuli za chama zinafanyika na si kukaa na kupanga safu za viongozi mnaowataka,” alisema Makamba.
Pia aliwasisitiza UVCCM Morogoro mjini kuhakikisha wanafanya shughuli za chama kuanzia katika matawi, kwa lengo la kuhimiza wanachama wanakuwa hai kwa kulipa ada zao kila mwezi sambamba na kufanya vikao vyao kwa mujibu wa taratibu za chama.