MAMLAKA ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra), inatarajiwa kupandisha nauli kwa wanafunzi wa shule za sekondari kwa kuwataka kulipa nusu ya nauli ya mtu mzima.
Hayo yalibainishwa jana na Rais wa Umoja wa Wanafunzi wa Shule za Sekondari Taifa, Silvester Kijingo, alipozungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) Dar es Salaam.
Alisema Sumatra imewaandikia barua na kuwajulisha kupanda kwa nauli hiyo kuanzia Julai mwakani na kusema kwamba nauli ya mwanafunzi wa shule ya msingi itaendelea kubaki sh 100.
Rais wa wanafunzi hao, alisema licha ya Sumatra kuwaandikia barua hiyo, lakini mpaka sasa wao kama wanafunzi hawana tamko lolote hadi hapo watakapowashirikisha wadau mwengine.
Alisema tatizo la nauli limekuwa kero kwao, lakini kipindi hiki wanataka ikifikie muafaka mzuri katika nauli za daladala na hata zile za mkoani na mjadala huo wa nauli watauibua baada ya kumaliza uchaguzi wa Rais katika shule za sekondari taifa.
Kijingo alieleza licha ya Sumatra kuwaruhusu wanafunzi kukaa kwenye viti kutokana na kulipa nauli ya sh 100, lakini tatizo bado lipo hasa kwa wanafunzi wa kike ambao wanakaa mbali na kupanda daladala zaidi ya moja.
“Lakini kuna wanafunzi wengine wanadandia malori ya mchanga na hawa ni wale wanaokaa mbali tena wanaishi katika mazingira magumu…na matokeo yake wanafunzi wengi ndoto zao zinapotea hasa pale wanapopewa ujauzito na hao madereva,” alisema Kijingo.