|
ZAIDI ya wanafunzi 200 wa kidato cha tano na sita wa Shule ya Sekondari ya Ufundi Moshi, wamelazimika kusitisha masomo yao kwa muda usiojulikana kutokana na upungufu wa chakula unaoikabili shule hiyo. Wanafunzi hao wanatakiwa kuondoka shuleni hapo kuanzia leo na kwamba watafahamishwa muda wa kurejea shuleni kupitia vyombo vya habari.
Kwa mujibu wa barua ya Mkuu wa Shule, Isack Malisa, iliyosainiwa na Makamu Mkuu wa Shule, Sigfrid Saweru, yenye kumbukumbu namba MTS/R.20/2/VOL.IV/59 ya Desemba 17 mwaka huu kwenda kwa wazazi wa wanafunzi hao, shule hiyo itafungwa rasmi leo. Katika barua hiyo, mkuu huyo wa shule alisema uongozi wa shule hiyo hautaruhusu mwanafunzi yeyote kubaki shuleni kwa muda wote ambao shule itakuwa imefungwa. “Imetulazimu kufunga shule kwa sababu ya ukosefu wa chakula; utakaa na mwanao hadi itakavyotangazwa mwakani kupitia vyombo vya habari kuwa shule inafunguliwa na hatutamruhusu mwananfunzi yeyote kubaki shuleni wakati wa likizo,” ilieleza barua hiyo. Hata hivyo, baadhi ya walimu waliozungumza na Tanzania Daima kwa masharti ya kutotajwa majina, walisema hali hiyo inatokana na serikali kushindwa kuwalipa wazabuni ambao wanadai zaidi ya sh milioni 150 kutokana na huduma walizotoa. Walisema shule hiyo ina zaidi ya wazabuni saba na kwamba wote wanadai fedha kutokana na kutoa huduma mbalimbali za chakula kwa kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja sasa. Walimu hao walisema kufungwa kwa shule hiyo ni agizo la Wizara ya Elimu ya Mafunzo ya Ufundi kutokana na upungufu wa chakula unaozikabili baadhi ya shule za serikali. Kwa upande wao baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo, wameingiwa na hofu ya kutofanya mitihani yao ya kumaliza kidato cha sita inayotarajiwa kufanyika Februari 8 mwakani na pia wanahofia kutofanya vizuri kutokana na kuwa na muda mchache wa maandalizi. Walisema waliitaji kuendelea kubaki shuleni hapo kwa ajili ya maandalizi ya mtihani huo wa taifa hadi Desemba 22 wakati wakisubiri shule kufunguliwa Januari 3 mwakani.
|