SAKATA la malipo ya kampuni ya kufua umeme ya Dowans, limeingia hatua mpya baada ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Utawala Bora, Mathias Chikawe, kusema mawaziri wawili waliompinga Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja kutangaza serikali kuilipa kampuni hiyo, walikiuka utaratibu wa serikali. Aidha, amewataka mawaziri hao, Waziri wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta na Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, kuacha kutoa maelezo ya sekta zisizowahusu kwani si utaratibu wa utawala bora na ni kuwachanganya wananchi.